Alhamisi, 18 Desemba 2014

HATUA 10 ZA KUFANIKISHA MALENGO YAKO 2015.


Safari ya kufikia Mafanikio, katika malengo yoyote uliyojiwekea inaweza kuchukua muda mrefu au mfupi kulingana na ulivyojipanga na hatua unaochukua. 

Hatua zifuatazo zitakusaidia kufanikisha malengo utakayojiwekea kwa mwaka ujao wa 2015 kwa haraka zaidi.

1.UFASAHA WA LENGO


Ni lazima ufahamu matokeo ya kile unachotaka kufanya, nikimaanisha kuwa ni lazima uwe na picha halisi ya kile unachotaka kukifanikisha. Lazima ujue unataka nini au unataka kuwa nani.
Lengo lazima liwe wazi, lijulikane kabla hujaanza kuchukua hatua yoyote. Kwa maana nyingine huwezi kuanzisha safari pasipo kujua mwisho wa safari yako.
Unapokuwa na lengo mahususi ni rahisi kupanga mikakati ya kulifanikisha. Akili na mawazo huanza kuvutia vitu ambavyo vitarahisisha ufanikishaji wa lengo lako. Ni vema kujikita hasa kwa kile unachohitaji na kuachana na yale usiyoyahitaji. Kuielekeza akili yako kwenye mambo usiyoyataka utavutia fikra hasi na kukosa hamasa na msukumo wa kuchukua hatua zaidi za kuelekea kwenye malengo yako.

2. CHUKUA UAMUzI  THABITI

Baada ya kugundua lengo mahususi ni wakati wa kuchukua uamuzi mathubuti wa kufikia Malengo yako. Ni wakati wa kuamua kuwa unaenda kufanya kile unachotaka kufanya kwa moyo wako wote, nguvu zako zote na akili yako yote na kwamba ni lazima ufanikiwe kwa vyovyote vile. Uamuzi huu lazima uwe umetoka moyoni mwako na si shinikizo au ushawishi wa watu wengine.
Uamuzi thabiti unadhihirisha kuwa kitu ulichoamua kufanya unakipenda na kimo katika damu yako. Kwa kufanya kitu ambacho ni shauku ya moyo wako ni rahisi kwako kuzigeuza changamoto utakazokutana nazo  kuwa fursa zitakazokurahisishia safari ya kuyafikia Malengo yako. Hautoweza kukata tamaa kwa urahisi hata pale mambo yanapoonyesha kuwa magumu.

3.CHUKUA WAJIBU BINAFSI

Tambua kwamba uamuzi uliouchukua ni wako binafsi kwa hiyo uwe tayari kuyapokea mambo yote ya sasa na yajayo yatakayotokana na uamuzi uliouchukua. Upo tayari kubeba lawama au pongezi. Hakuna mtu ambaye utamlaumu kwa lolote litakalotokea, hakuna wa kumsingizia wala kumyooshea kidole. Changamoto zote utazitatua mwenyewe na utakapoanguka utasimama mwenyewe. Kwa maana nyingine, usitegemee sana msaada watu wengine.

4. JIAMINI

Kujiamini kunakuweka karibu na Malengo yako. Woga unakuweka mbali na Malengo yako. Kujiamini ni nyenzo kubwa katika kufanikisha Malengo yako. Kujiamini ni kushinda  vita kabla ya pambano. Jiamini na unachokifanya na utazipenda hatua zote unazochukua kuyafikia Malengo yako.

5. UNGANA KIHISIA NA KILE UNACHOTAKA KUFANIKISHA.

Vuta picha mbalimbali za kihisia kwa lengo unalotaka kulifanikisha na ujione kana kwamba tayari umeshafanikiwa. Kama hamu yako ni kuwa daktari jione kwamba umeshakuwa daktari jione kuwa uko katika chumba cha daktari unawahudumia wagonjwa wako kwa furaha na wao wanafurahia huduma yako. Kama unapenda kuwa mfanyabiashara mkubwa vuta picha kihisia ukijiona upo na wateja unawahudumia au una saini hundi ama unaadaa manunuzi ya bidhaa. Kwa kufanya hivi unaihadaa akili yako fichika (subconscious mind) ambayo haijui kutofautisha kati ya jambo halisi na lisilohalisi hivyo itakuweka katika mazingira yanayoendana na picha unayoijenga akilini na kuvutia mambo ambayo yatakurahisishia kufanikisha malengo yako.

6.TAMBUA CHA KUFANYA KUKUFIKISHA KATIKA MALENGO YAKO

Lazima ujuwe ni nini cha kufanya kukufikisha katika malengo yako. Kwa lugha nyingine ni hatua gani uchukue ili kufikia malengo yako.

7. JIWEKEE MPANGO KAzI

Mpango kazi unahusisha kulivunja lengo kuu katika malengo madogomadogo ili kuweka urahisi wa kufanikisha adhma yako. Hii ni pamoja na kujipangia muda maalumu wa kufanikisha lengo lako, na kupanga mikakati itakayokusaidia.  Bila kuwa na mpango kazi uliojiandalia wewe mwenyewe unajipunguzia uwezekano wa kuyafikia malengo yako kwa muda na wakati unaotakiwa. Pia kuna uwezekano wa kuhama kabisa kwenye lengo na kujikuta unaelekea kwenye lengo jingine kabisa ambalo hukulitegemea. Zaidi ya hayo, unapojiandalia mpango kazi unajipa hamasa binafsi ya kuwekeza akili, mawazo na nguvu zaidi katika malengo yako.
Ni muhimu kuwa na mpango kazi zaidi ya mmoja  yenye mikakati tofauti ili usipoteze mwelekeo pale mpango mkuu unapofeli. (mfano Plan A, Plan B, Plan C, nk).

8. CHUKUA HATUA

Baada ya kujua nini cha kufanya, na kujiandalia mpango kazi, anza mara moja kuchukua hatua, hakuna haja ya kusubiri kila kitu kiwe tayari. Kumbuka, safari ya maili elfu moja huanza na hatua moja. Anza na ulichonacho hata kama hakijatimia na utaona hatua nyingine zinajiongeza zenyewe. Utaanza kuona njia inafunguka na kukuonyesha mwelekeo. Chukua hatua sasa! Bila kuchukua hatua yoyote itakuwa vigumu kufikia Malengo yako. Kumbuka kuwa pamoja na kuwa na mipango, mikakati na malengo mazuri, bila kuchukua hatua madhubuti hakuna kitakachoemdelea.

9.JITATHMINI

Je, hatua ulizochukua zinakupeleka karibu na Malengo yako au nje ya Malengo. Kama hatua unazochukua zinakuelekeza katika kufanikisha Malengo yako, basi endelea kuchukua na kuboresha hatua hizo. Lakini kama hatua unazochukua zinakupeleka nje ya Malengo yako jibu siyo kubadili Malengo……
Jibu ni……..

10. BADILI MIKAKATI

Badili mikakati na hatua unazochukua kuelekea katika malengo yako.
Na kama bado haikupelekei kuyafikia Malengo yako……….
Badili mikakati na hatua unazochukua.
Na kama bado haikupelekei kuyafikia Malengo yako……….
Tumia Plan B.
Na kama bado haikupelekei kuyafikia Malengo yako……….
Tumia Plan C.
Na kama bado haikupelekei kuyafikia Malengo yako……….
Endelea kubadili mikakati yako, Mpaka utakapofanikiwa.
Hakuna kukata tamaa, hakuna kurudi nyuma.

Kila la kheri. 

Jumatano, 17 Desemba 2014

UMEJIANDAAJE KISAIKOLOJIA KUFIKIA MALENGO YAKO?



 Washauri wa maendeleo binafsi  (Self Development)  wanatuambia  kwamba mikakati (strategies) huchangia asilimia 20 tu ya mafanikio ya mtu. Asilimia 80 hutokana na maandalizi ya kisaikolojia.

Hii ina maana kwamba maandalizi bora ya kisaikolojia ndiyo huchukua nafasi kubwa katika kufanikisha malengo yako.
Lakini wengi wetu tunakwenda kinyume. Tunapanga mikakati 100% na kusahau kabisa suala la saikolojia na wengine hatuna kabisa habari na kitu hiki. 
Tunafikiri kwamba tukiwa na mikakati mizuri tu tutafanikiwa.

Mikakati inaposhindwa kukufikisha kwenye malengo, unaanza lawama; “sina bahati… nimehujumiwa…serikali yetu haina sapoti…” tunalaumu ndugu na jamaa, tunalaumu wafanyakazi wenzetu, tunalaumu ndugu na jamaa na marafiki.

Hatutaki kuwajibika na matokeo yetu. Badala ya kukubali mapungufu yetu, kuzipokea changamoto na kuzifanyia kazi,  tunatafuta mchawi wa kumbebesha mzigo wa lawama.
Na kisha tunajiridisha kwa kuwachukulia wale waliofanikiwa kuwa hawakutumia njia halali. Wamehonga, wametoa rushwa, washirikina, mafreemason nk. 

Kuanguka au kufanikiwa kwa mtu huanzia kwenye fikra zake. 

Haijalishi askari ana mbinu kali au silaha bora kiasi gani, akiingia vitani na fikra za kushindwa, atashindwa tu.

Fikra ndio kila kitu. Weka fikra chanya kwenye malengo yako utaona mikakati inafanya kazi. Weka fikra hasi, utaona mikakati inakwama.

Mikakati ni nyenzo tu za kukuwezesha kuyafikia malengo yako. Nyezo pekee yake haziwezi kukufikisha unakotaka kwenda kama haukotayari au hujajiandaa kisaikolojia.

 Fikiria kuwa unataka kwenda ghorofa ya kumi na ngazi ndiyo nyenzo pekee ya kukufikisha, bila kujiandaa kisaikolojia utapataje msukumo na nguvu ya kupanda hizo ngazi?

Kuna maandalizi mengi ya kisaikolojia, hapa nitagusia baadhi tu.

       Uchu/shauku. Moyo wako ukitawaliwa na shauku kali ya kufanikisha malengo yako utakuwa na nguvu na msukumo wa kimwili na kiakili wa kuitumia  mikakati yako kukufikisha kwenye malengo yako.

Bila kuwa na uchu/shauku kubwa ni rahisi kukata tamaa na kuvunjika moyo endapo utakutana na vikwazo hata kama ni vidgo tu. Hutakuwa na moyo wa kupambana.

      Kujiamini. Jiamini wewe mwenyewe kuwa unaweza na kile unachokitaka kuwa kinawezekana. Unapojiamini unakuwa na nguvu na unajiweka karibu na malengo yako.
Unapokuwa na hofu unakuwa dhaifu na unajiweka mbali na malengo yako. Kujiamini ni kuwa na mtazamo chanya wa kufanikiwa kwa kile unachokifanya.

      Imani.  Ondoa imani zote potofu juu ya kile unachokitaka. Unapokuwa na imani zinazokinzana baina ya fikra na malengo,  si rahisi kufanikiwa. Kwa mfano, watu wengi tuna imani potofu kuhusu pesa ilihali tunazitaka kwa hali na mali. Methali hizi kuhusu pesa zinakinzana;  pesa asali ya roho/pesa chanzo cha matatizo.
Watu wengi tunaamini kuwa pesa hupatikana kwa kazi ngumu.  Imani hujenga. Ukiamini kuwa pesa ni ngumu basi itaendelea kuwa ngumu. Ukiamini kuwa pesa ni rahisi itakuwa rahisi tu. Ni imani tu. Ukiamini unaweza, utaweza. Ukiamini huwezi hutoweza kamwe.

Kwa ujumla, bila kuwa na maandalizi mazuri ya kisaikolojia, mikakati pekee haitasaidia kukufikisha unakotaka. Ni muhimu kuwa na mikakati mizuri na maandalizi mazuri ya kisaikolojia tunapopanga kufanikisha malengo yetu.


Mungu akubariki.

Jumanne, 16 Desemba 2014

UNAPAMBANA VIPI NA CHANGAMOTO ?


Unapowasikiliza watu waliofanikiwa kutimiza malengo yao kitu kikubwa wanachojivunia ni namna walivyozipokea na kuzifanyia kazi changamoto walizokutana nazo.

Watu hawa huzipokea changamoto kama baraka, wakiamini kuwa nyuma ya changamoto hizi  zimejificha fursa kubwa zinazopelekea ufumbuzi wa jambo wanalolishughulikia.

Hakuna fursa inayojitokeza waziwazi. Fursa huja zikiwa zimejificha nyuma ya changamoto. Utayari wako na moyo wa ujasiri wa kupambana na changamoto hizo ndiyo kutawezesha kuibua fursa nyingi zitakazo kuletea  mafanikio.

Watu wengi tunashindwa kufikia mafanikio ya kweli kwa sababu  tunazipokea changamoto kwa mtazamo hasi. Tunazipokea changamoto kama mikosi, laana au balaa fulani.

Tumesikia watu wengi wakijinyonga baada ya kufeli mitihani, wengine wakijiua baada ya kufukuzwa kazi, wengine wakinywa sumu baada ya kuachwa na wapenzi wao, na wengine wakikata tamaa kabisa baada ya kufilisika kibiashara.

Pengine kulikuwa na fursa kubwa nyuma ya changamoto hizo endapo watu hawa wangejipa ujasiri kidogo na kuzikabili changamoto hizo kwa mtazamo chanya. Nani anajua?

Kuna usemi maarufu usemao kuwa “changamoto zipo kwa ajili ya binadamu”. Ninavyoamini kila changamoto huwa na sababu ndani yake. 
Maendeleo yoyote unayoyaona leo duniani yametokana na changamoto zilizoshughulikiwa na watu. Kama kila mtu angekuwa anakimbia changamoto anazokutana nazo naamini kusingekuwa na maendeleo yoyote duniani.


Tusingekuwa na viongozi wakubwa duniani kama wasingekutana na changamoto kubwa. Alexander The Great, Napoleon, Mandela, Nyerere, taja na wengine unaowajua,wanajulikana na kuheshimika sana duniani kwa ujasiri wao wa kuzikabili changamoto walizokutana nazo.

Watu maarufu na matajiri wakubwa duniani wote walikutana na joto la changamoto kibao kabla hawajaanza kufurahia matunda ya uvumilivu wao.

Niliwahi kusikia kuwa Thomas Edson alifanya zaidi ya majaribio elfu moja kabla hajagundua taa ya umeme (light bulb). Angekata tamaa pengine tungekuwa bado gizani.

Ukimwangalia Oprah Winfrey leo huwezi kufikiri kuwa alizaliwa na kulelewa na mama yake tu, katika mazingira duni ya kijijini huko Mississippi Marekani, au aliwahi kuzaa akiwa na miaka 14 tu (bahati mbaya mtoto alifariki akiwa bado mchanga).
Akiwa mtoto Oprah alivaa nguo zilizotengenezwa kwa magunia ya viazi, ndivyo ambavyo familia yake ilimudu. Lakini leo je? Oprah ni mwanamke mwenye ushawishi mkubwa Duniani, akimiliki media empire,  jina kumbwa  na utajiri mkubwa. Huwezi kumkuta tena amevaa magunia ya viazi, labda kama itakuwa ni sehemu ya fasheni!

Steve Wonder alizaliwa kipofu, lakini hiyo haikumzuia kuwa mwanamuziki mwenye mafanikio makubwa nchini Marekani, akishinda grammy awards 22 ndani ya miaka 51 aliyoitumikia katika muziki.

umewahi kumsikia Legson Kayira? Ni Professor Maarufu wa Cambrige University. Alizaliwa Malawi katika jamii masikini kupindukia. Alitembea kwa miguu umbali wa zaidi ya maili 3000 kutoka Malawi hadi Cairo Misri kutafuta usafiri (meli) wa kuelekea Marekani akiwa hana hata senti, Baada ya kusoma na kuhamasishwa na kitabu cha historia ya Abraham Lincoln.  Kutokana na moyo wa kijasiri alifanikiwa kupambana na changamoto nyingi hadi kufika Marekani na kupata elimu aliyoitaka. yaliyofuata ni historia!!!

Pamoja na changamoto nyingi za enzi za ubaguzi wa rangi nchini afrika kusini, Nelson Mandela alifanikiwa kusoma sheria japo ilikuwa ngumu sana chini ya mfumo huu wa kibaguzi kwa Mwafrika kusomea mambo ya sheria. Mandela aliitumia taaluma yake ya sheria kuwatetea waafrika wenzake katika mfumo wa kibaguzi. Mandela alifungwa kwa kosa lakuupinga mfumo wa kibaguzi miaka ya 1960 .Baada yakutoka gerezani alikofungwa kwa miaka 27 Mandela alifanikiwa kuukomesha mfumo huu wa kibaguzi na kuleta utawala wa kidemokrasia nchini Afrika Kusini.

Wapo wengi sana waliopitia changamoto kubwa kama hizi ambazo baadae zilizaa neema na kuwanufaisha watu. Watu hawa hawakuwa na tofauti na mimi au wewe zaidi ya ujasiri na kutokata tamaa. 

Bila changamoto hakuna Mafanikio.

Jibu ni kupambana tu. Kwani, hata wewe unaweza!



NGUVU YA MALENGO

Katika Kufikia Mafanikio.

Katika kitabu  cha “The Great Escape”,  mwandishi Geoff Thompson anazungumzia kitu kimoja kilichonigusa na  kuamua kukileta kwako, huenda kwa namna moja au nyingine kikakugusa pia. Kifupi anazungumzia nguvu ya malengo katika kufikia mafanikio.

Geoff , anazungumzia survey maarufu iliyofanyika miaka mingi ya nyuma katika chuo kikuu cha Harvard, miongoni mwa vyuo bora zaidi duniani. Survey ilihusu mambo mbalimbali ambayo mwanafunzi alitakiwa kuyatolea maoni yake. Matokeo ya survey hiyo yalisababisha mshituko mkubwa miongoni mwa wahadhiri wa Harvard hususani katika vipengere vifuatavyo;

  1.                Una malengo?
  2.         Una utaratibu wa kuandika malengo yako? 

Karatasi zilipokusanywa na majibu kupitiwa, wahadhiri walishangazwa. Wastani wa 15% ya wanafunzi ndio waliojibu kuwa wana malengo yoyote, na kati  kati yao pia ni wachache tu ndio waliojaribu kuandika malengo yao.

Hii ina maanisha kuwa zaidi ya asilimia 85 ya wanafunzi wote waliofanyiwa survey, walikuwa wanasoma bila malengo yoyote. (Ikumbukwe kuwa Harvard hujivunia kudahili wanafunzi bora zaidi nchini Marekani).

Pamoja na kwamba survey hiyo iliwashangaza na kuwakatisha tamaa wahadhiri wa Harvad, matokeo yalihifadhiwa.

Miaka mingi baadaye, katika mkutano wa wafanyakazi wa chuo hicho, mhadhiri mmoja aliibua wazo la kurudiwa kwa survey kama hiyo ili kuona kama kuna tofauti ya wanafunzi waliokuwa wanadahiliwa muda huo na kipindi cha nyuma.

Kabla hawajakubaliana kuchukua survey nyingine ulifanyika uamuzi wa kukusanya pesa kwa ajili ya kuwafuatilia waliofanyiwa survey ya kwanza kama kuna walichofanikisha maishani.
Wanafunzi waliofanyiwa survey ya awali walitafutwa. Wale walioandika malengo yao waliulizwa;

Umefanikisha malengo uliyojiwekea kipindi ukiwa mwanafunzi?

Na wale ambao hawakuandika malengo yao waliulizwa;
Maisha yako yanaendaje?

Cha kushangaza, waligundua kuwa asilimia 95 ya wale ambao hawakuandika malengo yao hawakufanikiwa chochote na hawakuwa wamefikia uhuru wa kifedha kama ilivyokuwa inatarajiwa kwa mtu aliyehitimu chuo kikuu (hasa Harvard).

Asilimia 80 ya wale waliojiwekea malengo walikuwa wameyafanikisha na kwa wale wachache ambao waliandika malengo yao walikuwa wamekwisha fanikiwa kufikia uhuru wa kifedha.

Hapa tunajifunza kuwa kujiwekea malengo ni utaratibu muri wa kufanikiwa maishani.

Watu wengi tunapuuza kujiwekea malengo kwa kufikiri kuwa majina makubwa ya vyuo tunavyosoma yatatufanya tufanikiwe. Pengine kwa kudhani kwa kuwa tunafaulu mitihani yote tunayofanya, tutafanikiwa bila malengo kuwa na yoyote.

Au tunafikiri kuwa tutafanikiwa kwa kuwa tunatoka katika koo na familia maarufu.

Kwa vyovyote vile kujiwekea malengo ni muhimu kama unataka kufanikiwa.

Mtu asiye na malengo ni sawa na meli au ndege inayoanza safari bila kujua inakoelekea. Utawezaje kufika mahali ambapo hujui palipo? Huwezi kufika kama hujui unakokwenda.

 Unaweza ukaanzisha safari ndefu, ukavumilia dhoruba kali kwa kuwa unafahamu unakokwenda, unapaona unakoelekea. Hata kama mambo yatakuwa magumu vipi, utaangalia mbele na kusema, “ninaona mwnga mbele, nimekaribia kufika.”

Hebu fikiria unapigwa na dhoruba kali katika safari ambayo hujui unakoelekea, kishawishi cha  haraka kitakuwa ni kurudi ulikotoka au kuelekea sehemu nyingine. 

Bila malengo mbele utaona giza na maluweluwe tu. Watu wengi tunakata tamaa na kushindwa kufikia mafanikio kwa sababu hatuna malengo.


Unahitaji Malengo.